Kwa mujibu wa ripoti ya IQNA, Tovuti ya Al Ahram imeripoti kuwa, Dar al-Ifta ya Misri, inayoshughulikia masuala ya fatuwa za Kiislamu, imetangaza kuwa: "Mafundisho ya dini ya Kiislamu yanawahimiza Waislam kutoa salamu za pongezi kwa wasiokuwa Waislamu katika idi na minasaba yao ya kidini na hili ni kwa mujibu wa ubora wa tabia njema ambazo alikuja nazo Mtume SAW."
Dar al-Ifta ya Misri imeambatanisha taarifa hiyo na ujumbe wa video kuhusu kuwapatia wafuasi wa dini zingine salamu za pongezi kwa munasaba wa kumbukumbu za kuzaliwa manabii wao. Dar al-Ifta ya Misri imesema Uislamu ni dini inayowahimiza watu kuishi pamoja kwa maelewano na kwamba hakuna kosa kuwapa wasiokuwa Waislamu zawadi na kupokea zawadi zao kwa minasaba hiyo.
Dar al-Ifta ya Misri imeongeza kuwa kumbukumbu za uzawa wa Manabii wa Mwenyezi Mungu ni kheri na amani kwa wanaadamu wote na Uislamu ni dini ya amani, rehema, ubora na watu kutembeleana na kujuliana hali. Aidha ujumbe huo umeashiria Aya ya 107 ya Suratul Anbiyaa isemayo: "Nasi hatukukutuma ila uwe ni Rehema kwa walimwengu wote."
Katika ujumbe wake wa video, Dar al-Ifta ya Misri imetoa wito kwa Waislamu kufuatia Sira ya Mtume Muhammad SAW na kuwataka wasitumbukie katika mitego ya makundi ya wenye misimamo mikali ya kufurutu ada ambao wanawakufurisha wale wote wasioafiki fikra zao finyu.