IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu katika ujumbe kwa Mahujaji

Muamala wa Karne utasambaratika kwa hima na imani ya mrengo wa muqawama

12:05 - August 10, 2019
Habari ID: 3472077
TEHRAN (IQNA) – Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Sayyid Ali Khamenei ametoa wito kwa mataifa ya Waislamu kuungana kukabiliana na njama ya Marekani ya kile inachokitaja kuwa eti ni 'Muamala wa Karne' kuhusu kadhia ya Palestina.

Ayatullah Khamenei ameyasema hayo katika ujumbe uliotangazwa leo Jumamosi kwa Mahujaji wa Baitullahi Al Haram ambapo amesisitiza kuwa, dhulma kubwa zaidi katika karne za karibuni imejiri huko Palestina.

Ifuatayo ni matini kamili ya Ujumbe wa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu kwa Kongamano Kubwa la Hija

Kwa Jina la Allah Mwingi wa Rehema Mwenye Kurehemu

Na hamdu na shukrani zote zinamstahikia Allah, Mola Mlezi wa viumbe wote. Na rehema na amani ziwe juu ya Bwana wetu Mtume wa Mwenyezi Mungu, Mkarimu, na Mwaminifu, Muhammad Mtume wa Mwisho, na Aal zake watoharifu na hasa salio la Mwenyezi Mungu kwenye ardhi , na masahaba wake wateule na wote waliowafuata hao kwa wema hadi Siku ya Kiyama.

Msimu wa Hija kila mwaka ni mahali pa miadi ya rehema ya Mwenyezi Mungu kwa Umma wa Kiislamu.

Wito wa Qurani Tukufu wa  « وَ اَذِّن فِي النّاسِ بِالحَج»،  "Na watangazie watu Hija", ni mwaliko kwa watu wote katika kipindi chote cha historia kufika katika ugeni huu wa rehema ili nafsi na  roho ya kumtafuta Mwenyezi Mungu na pia mtazamo, na fikra zao zenye hekima ziweze kunufaika na baraka zake; na ili kila mwaka darsa na mafundisho ya Hija yaweze kufikishwa na kundi la watu kote katika Ulimwengu wa Kiislamu.

Katika Hija, kioevu cha dhikri na ibada, ambazo ni nukta asili katika malezi,ustawi na ubora wa mtu na jamii, pembizoni mwa mjumuiko na umoja ambao ni nembo ya umma mmoja, pamoja na harakati ya kuzunguka katika kituo kimoja na katika njia ambayo ina lengo la pamoja ambayo ni siri ya jitihada na harakati ya umma ambao msingi wake ni Tauhidi, na kuwepo katika kituo kimoja wote wanaotekeleza Hija na kutokuwepo tofauti baina yao, nukta ambayo inaonyesha kuondolewa kila aina ya ubaguzi na kuzifanya fursa zote kuwa sawa, yote hayo yanaonyesha mfano mdogo wa majmui ya misingi asili ya jamii ya Kiislamu. Ihramu, kutufu, sai, wuquf, rami , harakati na utulivu katika amali za Hija, ni ishara za kinembo za sehemu ya taswira ambayo Uislamu umewasilisha kuhusu mjumuiko wake  unaofaa.

Kubadilishana fikra na walivyonavyo watu wa nchi na maeneo tafauti ya mbali, kubadilishana habari na uzoefu, na kujuliana hali,kuondoa sutafahamu, kukurubisha nyoyo, kuleta pamoja nguvu na uwezo ili kukabiliana na adui wa pamoja, yote hayo ni mafanikio makubwa na muhimu ya Hija ambayo hayawezi kupatikana katika mamia ya mikutano mingine ya kawaida.

Amali ya kujibari na kujiweka mbali na mushirikina ambayo maana yake ni kuchukizwa na kila aina ya uonevu, udhalimu, ubaya, ufisadi wa mataghuti wa zama zote, na kusimama kidete mbele ya wanaotumia mabavu, na mustakbirina  wa zama hizi, ni moja kati ya baraka za Hija na fursa kwa Waislamu ambao mataifa yao yanadhulumiwa.

Leo kujiweka mbali na mrengo wa shirki na kufri, ambao ni mrengo wa mustakbirina, kinara wake akiwa ni Marekani, kuna maana ya kujiweka mbali na mauaji yanayotekelezwa dhidi ya wanaodhulumiwa na pia kuna maana ya kujiweka mbali na uenezaji vita; kuna maana ya kulaani vitovu vya ugaidi kama ule ugaidi  wa Daesh (ISIS) na Blackwater ya Marekani; kuna maana ya umma wa Kiislamu kueneza hofu na wahka katika utawala wa Kizayuni na waitifaki wake, huu ni utawala wenye kuua watoto; kuna maana ya kulaani sera za kupenda vita za Marekani na waitifaki wake katika eneo nyeti la Asia Magharibi na Afrika Kaskazini ambalo mataifa yake yamekumbwa na masaibu na matatizo na kila siku yanakabiliwa na maafa makubwa; kuna maana ya kuchukizwa na ubaguzi kwa msingi wa jiografia, kaumu au rangi ya ngozi; kuna maana ya kuchukizwa na tabia za kiistikbari na khabithi za  madola makubwa vamizi na fitina zinazotekelezwa dhidi ya wale wenye uungwana na uadilifu ambao Uislamu unataka wote wafuate.

Nukta hizo ni sehemu tu ya baraka za Hija ya Kiibrahimu ambayo, Uislamu halisi umetutaka kuitekeleza; na hii ni nembo ya sehemu muhimu ya malengo ya jamii ya Kiislamu ambayo kila mwaka, kupitia Waislamu katika Ibada ya Hija, huleta maonyesho adhimu yaliyojaa madhumini na kwa lugha inayoeleweka na ya kimantiki. Uislamu unawataka wote kujitahidi ili kuibua jamii kama hiyo.

Wasomi wa Ulimwengu wa Kiislamu, ambao baadhi yao kutoka nchi mbali mbali hivi sasa wanashiriki katika Hija, wana jukumu zito na muhimu katika mabega yao. Wasomi wanapaswa kufanya hima na kutumia ubunifu kufikisha haya mafunzo kwa mataifa na fikra za umma ili waweze kuibua mabadilishano ya kimaanawi ya fikra na pia mabadilishano ya motisha, uzoefu na ujuzi.

Leo kadhia muhimu zaidi katika Ulimwengu wa Kiislamu ni kadhia ya Palestina ambayo ni ya kwanza katika kadhia zote za kisiasa za Waislamu wa madhehebu, rangi na lugha zote.

Dhulma kubwa zaidi katika karne za karibuni imejiri huko Palestina. Katika tukio hilo chungu, kila kitu cha  taifa hilo, yaani ardhi yake, nyumba, mashamba na utajiri wake, heshima na utambulisho wake, vimeporwa. Taifa hili, kwa Taufiki yake Mwenyezi Mungu, halijakubali kushindwa na wala halikukaa kuwa mtazamaji na hivyo leo limejitokeza kwa ushujaa zaidi katika medani zaidi ya siku za nyuma; lakini ili mafanikio yapatikane kunahitajika msaada wa Waislamu wote.

Hadaa ya 'Muamala wa Karne' ambayo inaandaliwa na dola dhalimu la Marekani pamoja na wahaini wanaoandamana naye, ni jinai ambayo si dhidi ya haki ya taifa la Palestina pekee bali pia ni dhidi ya jamii nzima ya wanadamu. Tunatoa wito sote tujitokeze na tuchukue hatua za kivitendo ili kuvunja njama na vitimbi vya adui, na kwa uwezo wake Mwenyezi Mungu, njama hiyo na hila zingine zote za mrengo wa uistikbari zitasambaratishwa katika makabiliano na hima pamoja na imani ya mrengo wa muqawama na mapambano. Amesema Mwenyezi Mungu Azizi:

اَم يُ‍ريدونَ كَيدًا فَالَّذينَ كَـفَروا هُمُ ال‍مَكيدون

Au wanataka kufanya vitimbi tu? Lakini hao walio kufuru ndio watakao tegeka.

Namuomba Mwenyezi Mungu awajaalie Mahujaji wote taufiki, rehema na salama na awatakabalie Ibada yao.

Sayyid Ali Khamenei

Agosti 6 2019 (3 Dhu'l-Hijjah 1440)

 

captcha