Sheikh Ahmed Amer, qarii mwandamizi na Ustadh mashuhuri wa Qur’ani Misri na dunia nzima ameaga duniaakiwa na umri wa miaka 89.
Sheikh Amer alizaliwa mwaka 1927 katika mji wa Faqus katika jimbo la Ash Sharqiya nchini Misri ambapo alijifunza Qur’ani akiwa na umri mdogo. Aidha alipata mafunzo ya qiraa ya Qur’ani Tukufu na kubobea zaidi katika taaluma hiyo kadiri umri ulivyozidi kuongezeka.
Sheikh Amer alijiunga na Radio ya Misri kama qarii wa Qur’ani akiwa na umri wa miaka 36.
Sheikh Amer alitembelea nchi mbali mbali duniani kama vile Palestina, Brazil, Uingereza, Marekani, Ufaransa na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kushiriki katika vikao vya qiraa ya Qur’ani. Sheikh Amer kwa mara kadhaa alikuwa katika jopo la majaji wa mashindano ya kimatiafa ya Qur’ani nchini Iran.
Ameaga dunia wiki kadhaa baada ya qarii mwingine mashuhuri wa Misri, Sheikh Raghib Mustafa Ghalwash kuaga dunia Februari 4 akiwa na umri wa miaka 77.
Shirika la Habari za Qur'ani la Kimataifa (IQNA) linatoa salamu zake za rambirambi kwa jamii ya Qur'ani na Waislamu kote duniani kufuatia kuaga dunia quraa hawa wa Qur'ani.