IQNA

Madrassah ya Qur'ani yaharibiwa katika hujuma ya Al Shabab Mogadishu, Somalia

11:17 - September 03, 2018
Habari ID: 3471658
TEHRAN (IQNA)- Watu wasiopuingua sita wamepteza maisha na Madrassah ya Qur'ani kuharibiwa katika hujuma ya kundi la kigaidi la Al Shabab katika mji mkuu wa Somalia, Mogadishu.

Hujuma hiyo imejiri Jumapili asubuhi ambapo magaidi walikuwa wanalenga ofisi ya serikali za mitaa. Ofisi hiyo iliharibika kabisa na pia Madrassah ya Qur'ani iliyokuwa karibu nayo nayo pia imebomoka. Kati ya watu watatu waliopoteza maisha katika hujuma hiyo ni maafisa wa usalama waliojaribu kumzuia gaidi ambaye gari lake lilikuwa limesheheni bomu. Gaidi huyo alilipua gari lake lililokuwa limesheheni bomu karibu na lango la makao makuu ya Wilaya ya Hawldawag. Watu wengine waliouawa katika hujuma hiyo ni raia wa kawaida huku watu wengine 14, wakiwemo watoto sita wa Madrassah ya Qur'ani, wakijeruhiwa vibaya.

Kundi la kigaidi la al-Shabab kupitia msemaji wake, Abdiasis Abu Musab limetangaza kuhusika na hujuma hiyo. Magaidi wakufurishaji wa al-Shabab ambao aghalabu wanafungamana na mtandao wa kigaidi wa al-Qaeda wanaendesha kampeni ya mauaji kwa lengo la kuiangusha serikali ya Somalia yenye makao yake Mogadishu na ambayo inaungwa mkono na Umoja wa Mataifa.

Somalia ilitumbukia katika vita vya ndani mwaka 1991 na tokea wakati huo makundi mbali mbali yamekuwa yakipigana kuitawala nchi hiyo. Vikosi vya kulinda amani vya Umoja wa Afrika, maarufu kama AMISOM, havijaweza kurejesha amani kikamilifu nchini humo.

3466677

captcha