Katibu wa Mkuu wa Mkoa wa Karbala nchini Iraq amesema hadi kufikia Jumatatu zaidi ya wafanyaziara milioni 15 walikuwa wamewasili mkoani humo kwa lengo la kushiriki Arobaini ya Imam Hussein AS.
Mahfoudh At Tamimi amevieleza vyombo vya habari kuwa, katika ziara ya Arobaini ya mwaka huu, zaidi ya mazuwari milioni nne wasio Wairaqi tayari wameshawasili mjini Karbala kushiriki maombolezo ya Arobaini.
Wanazuoni wa madhehebu ya Shia wanasisitiza kuwa ziara ya Arobaini haishurutishwi kufanywa siku ya Arobaini yenyewe, kwa hivyo wafanyaziara Wairaqi na wasio Wairaqi huelekea Karbala kwa awamu siku kadhaa kabla ya Arobaini ili kufanya ziara ya Arobaini na kisha kurejea kwenye miji na nchi zao au kwenda kuzuru maeneo mengine matakatifu ya kidini nchini Iraq. Kwa msingi huo mwaka huu jumla ya wafanyaziara wa Arobaini ya Imam Hussein AS wanaweza kupindukia milioni 25.
Jumanne, tarehe 20 Mfunguo Tano, Safar mwaka 1440 hijria inayosadifiana na tarehe 30 Oktoba 2018 miladia ni Arobaini ya Imam Hussein AS, bwana wa vijana wa Peponi na mjukuu mpenzi wa Bwana Mtume Muhammad SAW, pamoja na wafuasi wake waaminifu. Kila mwaka mamilioni ya mazuwari aghalabu wakiwa Waislamu wa madhehebu ya Shia na pia Masunni pamoja na idadi kubwa ya wasiokuwa Waislamu kutoka kila pembe ya dunia huelekea mjini Karbala, Iraq kuzuru Haram toharifu ya Imam Hussein AS katika siku ya Arobaini yake.
Majlisi na ziara ya siku ya Arobaini hufanyika kila mwaka tarehe 20 Safar, kwa mujibu wa kalenda ya Hijria Qamaria, baada ya kupita siku Arobaini tangu tarehe 10 mwezi wa Muharram, kwa ajili ya kukumbuka siku aliyouawa shahidi mjukuu wa Mtume SAW, Imam Hussein AS na masahaba zake ambao walijitolea roho zao kwa ajili ya kuhuisha dini ya Mwenyezi Mungu katika jangwa la Karbala mwaka 61 Hijria Qamaria. Haram Takatifu ya Imam Hussein AS iko katika mji huo wa Karbala.
3471719