Taarifa zinasema katika hujuma ya Jumapili ,wanajeshi wa utawala wa Kizayuni walimuua kamanda wa ngazi za juu wa Brigedi za Ezzedin Al-Qassam, tawi la kijeshi la Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina, Hamas.
Kufuatia ukatili huo, Hamas imewaagiza wapiganaji wake kujiweka tayari kufuatia kuuliwa shahidi na kujeruhiwa wanamapambano wake. Duru zinasema Jumatatu jioni Hamas ilivurumisha maroketi kadhaa.
Hayo yanajiri wakati ambao hivi karibuni, mwanachama wa ngazi ya juu wa Hamas alitahadharisha kuwa baadhi ya nchi za Kiarabu zinaushawishi utawala wa Kizayuni utekeleze mashambulizi huko Ghaza.
Mahmoud al Zahar amesisitiza kuwa baadhi ya viongozi wa nchi za Kiarabu na Mahmoud Abbas Rais wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina wanaandaa mipango ili pamoja na kuishinikiza Hamas ibadilishane mateka, Israel iweze kutekeleza mashambulizi katika Ukanda wa Ghaza. Al Zahar hakutoa maelezo zaidi kuhusu mpango huo wa nchi za Kiarabu hata hivyo amesema kuwa baadhi ya hatua za Mahmoud Abbas kama kusitisha kuhamishia fedha katika mabenki ya Ghaza zinatekelezwa kwa lengo la kuwafanya wakazi wa eneo hilo kuwa dhidi ya Hamas.
3467196