IQNA

Rais Putin wa Russia atumia aya za Qurani kutoa wito wa amani Yemen

13:03 - September 17, 2019
Habari ID: 3472133
TEHRAN (IQNA) – Rais Vladimir Putin wa Russia amenukulu aya kadhaa za Qur'ani Tukufu katika kutoa wito wa kumalizika vita dhidi ya Yemen ambavyo vilianzishwa miaka mitano iliyopita na muungano wa kijeshi unaoongozwa na Saudi Arabia.

Akizungumza huko Ankara Uturuki Jumatatu akiwa ameandamana na marais Recep Tayyip Erdogan wa Uturuki na Hassan Rouhani wa Iran, Putini alinukulu sehemu ya aya ya 103 ya Sura ya Aal Imran katika  Qur'ani Tukufu isemayo…."Na kumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu iliyo juu yenu: vile mlivyo kuwa nyinyi kwa nyinyi maadui naye akaziunganisha nyoyo zenu; kwa neema yake mkawa ndugu."

Rais Putin amesema yale yanayojiri Yemen ni maafa makubwa ya kibinadamu na kuongeza kuwa kila ambaye ataweza kusaidia katika kuutatua mgogoro huo atakuwa amefanya kazi muhimu sana. Amesema njia bora zaidi ya kutatua mgogoro wa Yemen ni mapatano baina ya wahusika wote katika mgogoro huo.  Amesema mgogoro wa Yemen unapaswa kutatuliwa kwa msingi wa aya ya Qur'ani aliyoitaja hasa sisitizo la suala la udugu.

Rais Putin akiendelea kuashiria kuhusu uvamizi dhidi ya Yemen, amekumbusha pia kuhusu aya ya 190 ya Surah Al Baqara katika Qur'ani Tukufu isemayo: "Na piganeni katika Njia ya Mwenyeji Mungu na wale wanao kupigeni, wala msianze uadui. Kwani Mwenyezi Mungu hawapendi waanzao uadui."

Amesema kwa kuzingatia aya hizo, Saudi Arabia inapaswa kuchukua maamuzi muhimuna ya kimantiki.

Muungano wa kijeshi wa Saudi Arabia, ukipata himaya ya Marekani, Uingereza na utawala wa Israel ulianzisha uvamizi wake wa kijeshi dhidi ya Yemen mnamo mwezi Machi mwaka 2015.  Kufuatia vita hivyo vya Saudia dhidi ya taifa la Yemen, zaidi ya raia 17,000 wasio na hatia wameshapoteza maisha katika hujuma ya kinyama ya Saudia dhidi ya Yemen. Aidha muungano vamizi wa kijeshi unaoongozwa na utawala wa Saudia hutekeleza mashambulizi dhidi ya skuli, hospitali, maeneo ya makaazi ya raia, barabara, masoko, misikiti, madaraja, mabwawa ya maji safi, misafara ya mazishi na sherehe za harusi kote Yemen. Halikadhalika kutokana na hujuma hiyo ya Saudia dhidi ya Yemen, nchi hiyo sasa inakabiliwa na maafa makubwa zaidi ya kibinadamu duniani.

Lengo kuu la hujuma ya Saudia kuihujumu Yemen ni kumrejesha madarakani kibaraka wake, Rais mtoro wa nchi hiyo aliyejiuzulu Abd Rabu Mansour Hadi na kuwaondoa madarakani wanamapinduzi wa Ansarullah.

/3842671

captcha