Akizungumza na waandishi habari Antonio Guterres, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amebainisha masikitiko yake kuhusu kuendelea masaibu ya Waislamu wa jamii ya Rohingya ambayo aghalabu wanaishi katika kambi za wakimbizi katika nchi jirani ya Bangladesh. Amesisitiza kuwa lazima serikali ya Myanmar iandae mazingira ya Warohingya kurejea katiak ardhi zao.
Tokea Agosti 25 2017 wakati Jeshi la Myanmar lilipoanzisha hujuma dhidi ya Waislamu katika jimbo la Rakhine, Waislamu zaidi ya elfu saba wameuawa kwa umati na makumi ya maelfu ya wengine elfu nane wamejeruhiwa.
Kufuatia hujuma hizo Waislamu wengi wa kabila la Rohingya nchini Myamnar wameuawa au kulazimika kuhama makazi yao na kuwa wakimbizi katika nchi za jirani kutokana na mashambulio ya Mabuddha wenye misimamo ya kufurutu mpaka wanaoungwa mkono na serikali ya nchi hiyo. Kuna karibu Waislamu milioni moja wa jamii ya Rohingya waliokimbilia hifadhi nchini Bangladesh.
Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa Zeid Ra'ad Al Hussein amesema kuwa uhalifu unaofanywa na Mabudha kwa himaya ya serikali nchini Myanmar dhidi ya Waislamu wa jamii ya Rohingya ni mauaji ya kimbari.
Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC, imesema inatafakari kuhusu kuanzisha uchunguzi kuhusu ukatili wanaotendewa Waislamu wa jamii ya Rohingya.