Rais Rouhani ameyasema hayo leo Jumatano katika kikao cha Baraza la Mawaziri ambapo ameongeza kuwa, leo iwapo taifa la Iran litaungana na kuwa kitu kimoja basi hivi karibuni litapata ushindi. Ameongeza kuwa waliokuwa wakipanga njama ya kuisambaratisha Iran na mfumo wake wa Kiislamu leo wenyewe wanakiri wazi kuwa wamegonga mwamba katika njama hizo na hili linaonyesha kuwa ushindi uko karibu.
Rais wa Iran ameendelea kusema kuwa, wakati taifa la Iran limeweza kusimama kwa muda wa miaka mitatu mkabala wa dola moja kubwa, serikali mpya ya dola hilo imetangaza wazi kuwa sera za miaka minne za utawala uliotangulia zimefeli na kukiri huko ni ushindi kwa taifa la Iran.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema, kwa tadibiri, hatupaswi kuruhusu adui afikie malengo yake. Akiwahutubu watawala wa Marekani, Rais Rouhani amesema: "Msione haya, rejeeni katika mkondo wa sheria na msichelewe kutekeleza sheria za kimatiafa. Mfahamu pia kuwa, kama alivyosema Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, mtakaporejea katika utekelezaji wa ahadi zenu sisi pia tutatekeleza ahadi zetu."
Rais Rouhani katika mwanzo wa hotuba yake ametoa salamu za kheri na fanaka kwa kuwadia mnasaba wa Kubaathiwa Mtume Muhammad SAW na kuongeza kuwa, siku hii ni siku muhimu zaidi katika historia na kuongeza kuwa Uislamu ndio dini ambayo Mtume Muhammad SAW alitumwa kuieneza na maana ya dini hii ni amani na usalama na kusalimu amri mbele ya ya maamurisho ya Mwenyezi Mungu.