Katika siku ya kwanza ya mwezi mtukufu wa Ramadhani, mwezi iliyoshushwa
ndani yake Qur'ani Tukufu, Jumanne hii mjini Tehran kumefanyika - kwa muda wa
zaidi ya masaa matatu - mahfali na jalsa ya kuimarisha ukuruba na mapenzi na
Qur'ani Tukufu, mahfali ambayo imehudhuriwa na Ayatullah Udhma Sayyid Ali
Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu.
Katika mahfali na jalsa hiyo iliyojaa nuru na kuhinikiza uturi na manukato ya
kimaanawi ya Qur'ani Tukufu, maqarii na watu wanane waliohifadhi Qur'ani Tukufu
pamoja na wahadhiri wa Qur'ani kutoka pembe zote za Iran wamesoma machache
katika aya za maneno hayo matukufu ya Mwenyezi Mungu na kikundi kimoja cha
kusoma Qur'ani kwa pamoja kimepata fursa pia ya kusoma machache kutoka katika
kitabu hicho kitakatifu.
Katika jalsa na mahfali hiyo, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu
amesema kuwa, ujamali au umaridadi wa
maneno ya Qur'ani ni muujiza na ni dirisha la kuvutika watu upande wa kuelewa
vizuri mafundisho aali na yenye maana pana ya aya za Kitabu hicho kitukufu.
Aidha ameelezea ulazima wa kupewa umuhimu jalsa na vikao vya Qur'ani katika
kona zote za Iran na kugusia namna dunia leo hii inavyohitajia mno mafundisho
ya Qur'ani Tukufu kuliko jambo jingine lolote na kuliko wakati mwingine wowote
na kusema: Kama maana pana za Qur'ani Tukufu watabainishiwa watu kwa lugha
nyepesi ya kisasa bila ya shaka yoyote taathira za aya hizo zitakuwa kubwa na
zitaandaa uwanja wa kupatikana maendeleo ya kweli ya mwanadamu, kwani heshima,
nguvu na uwezo, ustawi wa kimaada, kuimarika kimaanawi, kuenea fikra na itikadi
na kupatikana furaha na utulivu wa moyoni, yote hayo yanategemea kiwango cha
kushikamana kwetu kivitendo na mafundisho ya Qur'ani Tukufu.
Mwanzoni mwa matamshi yake, Ayatullah Udhma Khamenei amewakumbuka kwa wema
maqari na wasomaji wa Qur'ani Tukufu waliotangulia mbele ya Mwenyezi Mungu
mwaka jana katika maafa ya Mina huko Saudi Arabia na sambamba na kuelezea
kufurahishwa kwake kwa kuona kuwa vijana wanazidi kushikamana na Qur'ani nchini
Iran amesema kuwa: Ijapokuwa ujamali au
umaridadi na mvuto wa maneno ya Qur'ani Tukufu ni muujiza, lakini lengo la
maneno hayo ni kufungua dirisha la kufikia kwenye anga iliyojaa baraka ya
mafundisho ya Qur'ani.
Amesisitiza kwamba: Kama mafundisho ya Qur'ani Tukufu yatapewa umuhimu
unaotakiwa, bila ya shaka yoyote kina na maana pana za aya za Qur'ani na
taathira zake zitakuwa kubwa zaidi katika dunia ya leo iliyo na mazonge mengi na
inayokabiliwa na tufani za matatizo na mashaka ya kila namna.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amelitaja suala la kuongezeka na
kuenea na kuimarika zaidi jalsa na mahfali za Qur'ani Tukufu nchini Iran kuliko
ilivyokuwa kabla ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu bali hata katika kipindi
cha mwanzoni mwa ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu kuwa ni jambo lenye ibra na
maana maalumu na kuongeza kuwa: Moja ya mambo ya lazima yanayopaswa kufanyika
nchini, ni kuenezwa na kuimarishwa zaidi vikao vya kusoma na kusikiliza Qur'ani
Tukufu.
Ayatullah Udhma Khamenei ameongeza kuwa: Kama vinavyofanyika vikao vya
maombolezo na vya furaha kuhusiana na Ahlul Bait (Alayhimus Salaam), vikao vya
Qur'ani Tukufu navyo inabidi vienezwe na kuimarishwa zaidi ili sambamba na kufanyika
jambo hilo, iweze kuongezeka kasi ya ustawi na ukuaji wa suala zima la
kushikamana na mafundisho ya Qur'ani Tukufu.
Vile vile amegusia namna dunia ilivyo na pengo la utambulisho, fikra na imani
na jinsi mwanadamu anavyohitajia mno mafundisho ya Qur'ani Tukufu kuliko wakati
mwingine wowote na kusisitiza kwamba: Inabidi tuiimarishe zaidi na zaidi
misingi yetu ya kiimani na kuwa na welewa wa kutosha kuhusiana na lugha
inayofaa ya kuyafikia kwa njia sahihi mafundisho ya Qur'ani Tukufu kwa watu
wengine ili kwa njia hiyo tuweze kuyatangaza vizuri mafundisho ya Kitabu hicho
kitukufu cha Mwenyezi Mungu.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza kuwa: Kama mafundisho ya
Qur'ani Tukufu yatafikishwa vizuri kwa watu, bila ya shaka yoyote yatakuwa na
taathira nzuri na kubwa sana duniani na wakati huo tena madola ya kibeberu na
silaha zao pamoja na utawala wa Kizayuni hawataweza kufanya ghalati na upuuzi
wowote ule.
Ayatullah Udhma Khamenei amesema pia kuwa, utulivu wa kiroho na kidini ni
miongoni mwa baraka nyingi za kuwa na welewa wa kutosha kuhusiana na mafundisho
ya Qur'ani Tukufu na kuongeza kwamba: Utulivu huo ndio unaoandaa uwanja wa
kuongezeka imani ya mtu kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu na kwa uwezo na nguvu zisizo
na kikomo za Allah.