IQNA

Kiongozi Muadhamu Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Serikali ifuate mwenendo wa Imam Ali AS

6:58 - June 24, 2016
Habari ID: 3470413
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amebainisha vipengee kadhaa vya hekima za Imam Ali bin Abi Twalib (as) zilizoandikwa katika kitabu cha Nahjul Balagha.

Ayatullah Udhma Sayyid Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu aliyasema hayo Jumatano jioni mjini Tehran, aliponana na Rais wa Jamhuri ya Kiislamu na wajumbe wa Baraza la Mawaziri la Iran ikiwa ni katika kuendeleza mialiko yake ya Ramadhani na futari kwa watu wa kada na daraja mbali mbali nchini. Kiongozi Muadhamu ametumia fursa hiyo kubainisha hekima kadhaa zilizomo kwenye kitabu cha Nahjul Balagha.
Ameashiria matamshi ya Amirul Muminin, Imam Ali (Alayhis Salaam) kuhusiana na namna watu wanavyopasa kufanya wakati inapotokea fitna na kusema: Imam Ali (Alayhis Salaam) anatuusia kwamba, wakati inapotokea fitina na ikawa ni jambo zito kutofautisha baina ya haki na batili, tuchukue hatua ambazo hazitaisaidia fitna kwa hali yoyote ile.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameongeza kuwa: Wakati inapotokezea fitna kama ile iliyotokea nchini Iran mwaka 2009, si sahihi kuruhusu masuala kama matamshi, kunyamaza kimya, uchukuaji hatua bali hata namna ya uangaliaji na utazamaji wa mambo, yasaidie kupata nguvu fitna.
Ayatullah Udhma Khamenei ameongeza kuwa: Tab'an inawezekana wakatokezea watu wakawa hawako tayari kujitokeza hadharani kukabiliana na fitna kutokana na mitazamo yao maalumu, lakini si sahihi kumtumia vibaya mtu huyo kwa ajili ya kukuza fitna hiyo.
Vile vile amegusia hekima nyingine ya Imam Ali (Alayhis Salaam) ndani ya Nahjul Balagha kwa kuzungumzia suala la kuangalia cheo kwa tamaa na kukiona kuwa ni fursa ya kujitajirisha na kupata upendeleo maalumu na kusema: Cheo ni dhamana, hivyo kuwa na mtazamo wa tamaa namna hiyo kuhusu cheo, hupelekea mtu kupoteza heshima yake na kudhalilika.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ametoa ufafanuzi zaidi kuhusiana na suala hilo kwa kugusia suala la baadhi ya watu waliotumia vyeo vyao kutwaa kiasi kikubwa cha mishahara na kusisitiza kwamba: Suala la mishahara mikubwa kupindukia kwa hakika ni kuhujumu matukufu ya nchi lakini kila mtu anapaswa kutambua kuwa, jambo hilo ni katika masuala ya nadra kutokea na kwamba sehemu kubwa ya wakuu na viongozi wa taasisi mbali mbali nchini ni watu wasafi. Hata hivyo, pamoja na kwamba watu waliofanya hivyo ni wachache lakini kitendo chao hicho ni kiovu na ni kibaya sana na lazima sheria ifuate mkondo wake kukabiliana nao.
Vile vile amegusia amri iliyotolewa na mheshimiwa Rais kwa Makamu wa Kwanza wa Rais ya kulifuatilia vilivyo suala hilo na kusema: Ufuatiliaji wa jambo hilo haupaswi kuchelewa, bali inabidi hatua kali zichukuliwe haraka na wananchi waelezwe matokeo yake.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameongeza kuwa: Kwa mujibu wa taarifa zilizonifikia, kiwango cha mishahara ya wakuu katika taasisi mbali mbali nchini ni cha kawaida na kinakubalika na kwamba wakuu wanaopokea mishahara mikubwa kupindukia ni wachache. Pamoja na hayo, hatua kali sana zinapaswa kuchukuliwa hata kama wakuu hao wanaochukua mishahara ya namna hiyo ni wachache sana.
Katika sehemu ya mwisho ya matamshi yake, Ayatullah Udhma Khamenei ameashiria hekima nyingine za Imam Ali (Alayhis Salaam) zilizomo ndani ya kitabu cha Nahjul Balagha na kusema: Inabidi kuchunga ndimi zetu wakati wote, kwani sehemu kubwa ya matatizo yanayomkumba mwanadamu huwa yanatokana na ulimi wake.
Amesisitiza kuwa: Matatizo yanayotokana na kutochunga ulimi wakati wa kuzungumza, baadhi ya wakati huwa yanaishia tu katika kupata madhara mtu mwenyewe aliyeshindwa kuchunga ulimi wake, lakini baadhi ya wakati jambo hilo huzusha matatizo katika jamii nzima, hivyo tunapaswa kuchukua tahadhari kubwa kuhusu suala hilo.
Kabla ya hotuba ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, Hujjatul Islam Walmuslimin Hassan Rouhani, Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ametoa ripoti fupi kuhusiana na hatua mbali mbali zilizochukuliwa na serikali yake na mipango na mikakati yake ya baadaye.
Mwishoni mwa mkutano huo, hadhirina wamesalishwa sala za Magharibi na Isha na Ayatullah Udhma Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu na baadaye wamekula futari pamoja naye.

3509730

captcha