Nakala hiyo ya Qur'ani Tukufu ambayo imepewa jina la Mus'haf Mashhad Razawi, umeandikwa kwa maandishi ya Hijazi, kutokana na kuwa uliandikwa katika eneo la Hijaz, Saudi Arabia.
Wataalamu wamethibitisha kuwa Msahafu huo uliandikwa katika karne ya kwanza ya kudhihiri Uislamu (Karne ya 7 Miladia).
Akihutubu katika hafla ya uzinduzi huo Alhamisi, mtafiti na mfasiri wa Qur'ani Tukufu Ustadh Murtadha Kariminia amesema Mus'haf Mashhad Razawi ni mjumuiko wa Misahafu miwili ambayo kila moja una sehemu ya Qur'ani Tukufu na kwa pamoja inajumuisha Qur'ani Tukufu. Amesema utafiti na uchunguzi kwa mbinu ya kaboni umebaini kuwa sehemu kubwa ya Msahafu huo uliandikwa katika karne ya kwanza Hijria. Msahafu huo uliandikwa katika vipanda vya Ngozi vya sentimita 35 kwa 50 ima mjini Madina au Kufa na kisha kuhamishiwa Khorassan (kaskazini mashariki mwa Iran) baadaye, amesema mataalamu huyo.
Amesema katika karne ya 5 Hijria, mmiliki wa Msahafu aliuzawadia Haram ya Imam Ridha (AS). Misahafu iliyoandikwa kwa maandishi ya Hijazi ni kati ya Misahafu mikongwe zaidi ambayo imesalia hadi sasa.