Kwa mujibu wa mwandishi wa IQNA, Ali Bakhtiari, mwambata wa utamaduni wa Iran nchini Uganda alitembelea kituo cha Radio Bilal ambapo alikutana na kufanya mazungumzo na mkurugenzi wa radio hiyo Musa Kirunda ambapo walijadili kuimarisha ushirikiano.
Mwanzoni mwa kikao hicho, Musa Kirunda alibainisha harakati za Radio Bilal na kusema kituo hicho kinajishughulisha katika kuuarifisha Uislamu katika kipindi cha miaka 10 iliyopita.
Amesema radio hiyo inasikika mashariki, magharibi na kusini mwa Uganda ambapo ina idadi kubwa ya wasikilizaji na katika siku za usoni itaenea katika maeneo ya kaskazini mwa nchi hiyo.
Katika kikao hicho Ali Bakhtiari aliarifisha Shirika la Utangazaji la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran IRIB na kusema Iran ni kati ya nchi zilizostawi katika uga wa habari. Amesema Iran ina idadi kubwa ya radio na televisheni za ndani ya nchi na pia za kimataifa ambazo hutangaza kwa lugha mbali mbali.
Amesema kuna haja ya kutumia vyombo vya habari kueneza ujumbe wa Uislamu sahihi na kuonyesha Uislamu kama dini ya amani.