IQNA

Tawfiq Allawi asema hataki nafasi ya waziri mkuu wa Iraq

14:36 - March 02, 2020
Habari ID: 3472522
TEHRAN (IQNA) - Mohammed Tawfiq Allawi, Waziri Mkuu wa Iraq ametangaza kujiondoa kuunda Baraza la Mawaziri la nchi hiyo.

Akizungumza kupitia mkanda wa video, Mohammed Tawfiq Allawi amesema kuwa, amechukua uamuzi huo kutokana na mashinikizo ya kisiasa ya baadhi ya makundi ya Iraq.

Mohammed Tawfiq Allawi amemuandikia pia barua Rais Barham Salih wa nchi hiyo akimuomba radhi kutokana na kushindwa kuunda serikali na hivyo ameamua kujivua jukumu hilo.

Rais Barham Salih wa Iraq amepokea na kuafikia barua ya Mohammed Tawfiq Allawi ya kujiondoa katika jukumu alilopewa kama Waziri Mkuu la kuunda serikali.

Rais wa Iraq amesema kuwa, kuwa, atamtangaza Waziri Mkuu mpya wa Iraq katika kipindi cha siku 15 zijazo baada ya kufanya mashauraino na vyama na mirengo mbalimbali ya kisiasa ya nchi hiyo.

Jana kikao cha Bunge la Iraq kkwa ajili ya kulipigia kura Baraza la Mawaziri la Mohammed Tawfiq Allawi kiliakhirishwa kwa mara ya tano kutokkana na kutotimia akidi. Muhula wa mwisho wa Mohammed Tawfiq Allawi wa kuunda serikali ulikuwa unamalizika leo.

Itakumbukwa kuwa aliyekuwa Waziri Mkuu wa Iraq Adil Abdul-Mahdi alijiuzulu wadhifa huo Novemba 30 mwaka uliopita kufuatia maandamano ya upinzani ya wananchi yaliyofanyika katika miji kadhaa ya nchi hiyo, na tangu baada ya kujiuzulu amekuwa akiongoza serikali ya mshikizo wakati nchi hiyo inangojea kuteuliwa Waziri Mkuu mpya.

3470801

captcha